Katika maisha yetu tunayoishi hakuna mtu hata mmoja, ambaye hana watu wanaompinga hata kama anafanya jambo jema.
Na wengi wanapokutana na fitina za watu hao hujiona hawafai na wanataka kukata tamaa kwa kile wanachofanya katika maisha.
Mara nyingi wamekuwa wanaumizwa na maneno yanayosemwa na watu hao kuwahusu wao.

Hebu tuangalie kitu gani ufanye pindi unapokabiliwa na mazingira kama hayo:

1.USIACHE KUJIPENDA:

Mahusiano yako na nafsi yako yanatakiwa uyaangalie kwa ukaribu sana kwa kujitunza,
kwani ndio msingi ambao maadui wanajitahidi kuubomoa kwanza.
Wakishafanikiwa kukufanya ukajichukia basi kazi ya kukuharibu 
inakuwa ni rahisi mno.
Hakuna mtu ambaye anajichukia yeye halafu akafanikiwa kuwa na mahusiano mazuri na wengine.

2.FANYA KILE NAFSI YAKO INAKWAMBIA NI SAHIHI:

Usiogope kutembea barabara ya peke yako, na usiogope kuelekeza nguvu zako huko kwasababu tu ya maneno ya watu wengine.
Usiruhusu ujinga, maigizo ya watu na fikra zao hasi zikufanye usifikie ndoto zako.
Endelea kufanya kile kitu moyo wako unakwambia ni sahihi na unafurahia.
Hii ni kwasababu pale wewe unapofanya kitu sahihi ambacho nafsi yako inapenda hakuna atakayeweza kukuangusha kirahisi. 

3.FUATA NJIA ZAKO:

Kila siku hapa duniani inatoa nafasi kwa kila binadamu kufanya mabadiliko katika maisha yake.
Jitahidi kuitumia kufanya mabadiliko unayoyatamani usiruhusu mtu mwengine akubebeshe mzigo usiouhitaji.
Fanya hayo ukijua wazi kuwa pamoja na kwamba kuna watu wanachukia, lakini pia kuna wengine wanapenda unachofanya.

4.FANYIA KAZI MALENGO YAKO:

Unatakiwa ufanyie kazi malengo yako makubwa na ambayo unaona yanatekelezeka hata kama kuna watu wanakwambia hayawezekani.
Tambua kuwa mafanikio yanakuja kwa kufanyia kazi malengo yako.
Ile shughuli ambayo unaipa muda mwingi kila siku ndiyo inayoamua wewe uwe nani, kwahiyo tumia muda mwingi katika kutimiza malengo yako.

5.BADILISHA LENGO PALE UNAPOONA MAZINGIRA YAMEBADILIKA:

Kuna kipindi unaweza ukapanga lengo la kufanya shughuli fulani kutokana na mazingira kufungua fursa na umeiona.
Lakini baada ya muda mazingira hayo yakabadilika, usiwe mgumu kutafuta lengo mbadala hata kama la mwanzo ulitumia muda mrefu kuliandaa japo kuna watu watakushauri usibadilike.
Maisha siku zote hayatabiriki, lakini yanafungua milango kwa watu kutimiza ndoto zao.

6.USIWE MTU WA VISASI:

Tumia muda wako mwingi kufanya mambo yako ya muhimu kuliko kukaa na kufikiria namna ya kumlipizia 
kisasi mtu aliyekukosea.
Wengi watakushawishi ufanye hivyo ili upoteze dira na mipango yako kwa kushughulika na maisha ya watu na kuacha kufanya mambo yako.

7.ONYESHA UKARIMU NA UPENDO KWA WATU:

Usiwe mtu unayechagua watu wa aina fulani, ndio wa kuwaonyesha upendo kwa kuwa wanamchango kwako.
Japo hata ukifanya mambo mema vipi bado kuna watu watakushauri uache.
Jitahidi kuwafanyia matendo ya upendo na ukarimu watu unaokutana nao, kwani ukweli ni kuwa vile unavyowatendea wao ndivyo na wewe utakavyotendewa.

8.TETEA WATU WANAO ONEWA:

Mara nyingi unakutana na watu usiowafahamu au unaowafahamu, wakiwa katika matatizo ya kunyanyaswa. 
Usiache kuwatetea pale unapoona una uwezo wa kutoa msaada na ukawatoa 
katika hilo tatizo.
Ukifanikiwa kufanya tendo kama hilo ndani yako unajengeka moyo wa kishujaa wa kujiona una mchango katika jamii yako 
na watu watakujali.



YAWEZEKANA KABISA UKAWA KATIKA ENEO AMBALO WATU WENGI WANAOKUZUNGUKA HAWAKUPI USHIRIKIANO WA VITU UNAVYOTAKA KUFANYA.

KWA KUPITIA MAMBO HAYO HAPO JUU UNAWEZA UKAWEZA KUPAMBANA NAYO NA MWISHO WA SIKU UKAWA MSHINDI.







Share this post:

Digg it StumbleUpon del.icio.us Google Yahoo! reddit

0 comments:

Post a Comment

 
Copyright 2013-2017 Lisha Ubongo
| Branded by www.pixelbase.co.tz