Ukikutana na mtafuta ajira kilio chake kikubwa ni nimefanyiwa usaili mara nyingi ila baada ya hapo sijaitwa tena.

Waajiri huwa wanatumia vigezo gani katika kujaza nafasi za kazi katika ofisi zao? Kama unadhani una jibu moja litakalo wawakilisha waajiri wote kutokana na swali hilo, naomba nikwambie tafakari Zaidi.


Waajiri wote si sawa, anachokitafuta mwajiri mmoja kinaweza kuwa tofauti na mwajiri mwengine. Sababu inaweza kuwa ni kuwa mazingira ya kazi ya mwajiri mmoja yanatofautiana na mwajiri mwengine, kwahiyo watakapokuwa wanakusaili watakuwa wanaangalia vitu tofauti kutoka kwako.

Kila mwajiri anatafuta stadi za mwombaji zitakazoendana na kazi alizonazo katika ofisi yake ili kuboresha ufanisi wa kazi ili kutoa bidhaa au huduma nzuri kwa wakati na ubora unaotarajiwa na mteja. Lakini nje ya stadi kuna vitu ambavyo waajiri wengi wanafanana katika kuviangalia kutoka kwa mwombaji wa ajira.


Habari nzuri ni kuwa watafuta ajira wengi wanazo hizo sifa ila tu wanashindwa kuzionyesha wanapopata nafasi ya kuzionyesha. Na habari nzuri Zaidi ni kuwa kwa wale ambao hawana wanaweza kujijengea tabia hizi na zikawapa nafasi nzuri ya kuajiriwa kwa kupata mtu sahihi wa kuwaelimisha.

Na habari nzuri Zaidi ni kuwa utakapozijua hizi tabia utaweza kuboresha mfumo wako wa uombaji kwa kuelekeza moja kwa moja katika wasifu wako kile anachotafuta mwajiri katika kazi husika. BAdala ya kujaza masifa kibao katika wasifu wako utajua namna ya kuweka zile za muhimu.


   1. UWEZO WA KUWASILIANA



Uwezo wa kuwasiliana upo katika pande tatu moja ni uwezo wa kusikiliza, pili ni uwezo kuongea na tatu ni uwezo wa kuandika. Na kama unavyojua lugha yetu ya kiofisi ni kiingereza sasa ukiwa vizuri katika pande hizo tatu utajiweka katika nafasi nzuri katika soko la ajira. 

Unapokuwa na uwezo wa kupokea maelekezo kwa haraka na kuyahamishia katika maandishi na ukaweza kueleza matokea yake iwe kwa maandishi au mdomo ufanisi kazini utakuwa juu. 

Utajisikiaje unampa maelekezo mfanyakazi wako jinsi ya kufanya kazi Fulani na akashindwa kufanya kama ulivyomuelekeza kisa hamuelewani lugha?

  2.UWEZO WA KUTUMIA KOMPYUTA



Hapa tuelewane vizuri, kujua kompyuta haimaanishi lazima uwe umesomea kozi yake miaka kadhaa chuo labda kama kazi unayoomba inahusiana moja kwa moja na uweledi wa kompyuta kwa kusomea kozi husika. Ila kama unaomba kazi ambazo hazina uhusiano wa moja kwa moja na masomo ya kompyuta, nataka nikwambie haimaanishi ndo usijue kitu kuhusu kompyuta. 

Dunia hii ya utandawazi kila kazi kwa namna moja ama nyingine ili kuikamilisha lazima kompyuta itaingia kati sasa kama hujui kuitumia kabisa utakuwa unajipunguzia soko. Mathalani uweze kutuma barua pepe (E-mail), programu ya maandishi (Microsoft word) na program ya namba na maandishi (Microsoft Excel)

  3.UWEZO WA KUBADILIKA/KUFANYA KAZI ZAIDI YA MOJA


Katika dunia hii ambayo ukuaji wa teknolojia na ushindani wa huduma na bidhaa umekuwa mkubwa ofisi nyingi hupunguza gharama kwa kuajiri watu wachache wenye uwezo wa kufanya kazi Zaidi ya moja ili gharama za kuzalisha ziwe ndogo na wao waweze kushusha bei kupunguza ushindani na kuliteka soko. 

Hivyo ukiwa na sifa ya uelewa wa kazi Zaidi ya moja utajiongezea nafasi katika soko la ajira.


  4.UWEZO WA KUCHANGANYIKA NA WENGINE



Katika mazingira ya ofisi ambayo binadamu Zaidi ya mmoja wanashirikiana kufanikisha lengo moja  la ofisi, uwezo wa mfanyakazi mmoja kuchangamana na mwengine bila tatizo ni jambo la muhimu sana. 

Ofisi inaweza kuruhusu mtofautiane kwa hoja ili kupata kitu kizuri lakini si kugombana sababu wazo la mmoja limepingwa na wengi na kuwanunia, hii italeta utengano na kushusha ufanisi mahali.

Ukiwa na uwezo wa kuchangamana na wengine mathalani katika wasifu wako ukaweza kuonyesha kwamba uliwahi kufanya kazi na watu Fulani na kufanikisha jambo Fulani.

  5.UWEZO WA KUONGOZA




Sehemu yoyote ambayo wanakutana watu Zaidi ya wawili lazima kuwe na kiongozi na lazima ujue miongoni mwenu lazima atoke kiongozi.

Waajiri wengi wanapenda mtu mwenye uwezo wa kuongoza sababu wenye tabia hii huwa na uwezo wa kufanya maamuzi ya kibunifu hivyo wanatarajia hata wakati wa utendaji wako utakuwa unafanya kwa ubunifu na kuwaongoza wengine  na si kufuata njia zile zile zilizopitiwa na wengine na hivyo kuongeza ufanisi kazini.

HAUJACHELEWA KUFANYA MAREKEBISHO PALE AMBAPO UNAONA UNA MAPUNGUFU ILI KUONGEZA UWEZO WAKO WA KUAJIRIKA KATIKA SOKO LA USHINDANI WA AJIRA.

HAKUNA ALIYEZALIWA NA SIFA ZOTE HIZO BALI WENGINE WAMEZITENGENEZA NA WAKAWEZA KUZIFANYA KUWA SEHEMU YA MAISHA YAO NA MATOKEO MAZURI WAKAYAPATA.

ANZA SASA KUPIGA HATUA...

Share this post:

Digg it StumbleUpon del.icio.us Google Yahoo! reddit

1 comments:

Anonymous

Nakubaliana na wewe. Ila labda ungekwenda mbali zaidi. Stadi za kazi zipo takribani 60. kwa kiingereza zinaitwa soft skills. Hizi hazifundishwi shuleni. Watu wote, na hata wale ambao sio waajiriwa wanatakiwa kujifunza na kuzifanyia mazoezi. Stadi yeyote hata zile zinazoitwa hard skills, lazima mtu ajufunze halfu aziafanyie mazoezi (practice). Tupo pamoja.

Post a Comment

 
Copyright 2013-2017 Lisha Ubongo
| Branded by www.pixelbase.co.tz