JINSI UNAVYOWEZA KUBORESHA MAHUSIANO YAKO KATIKA ENEO LA KAZI.



“Usimamizi wa ubora, usalama, hadhi, mahusiano, ushirikiano, na sera ya ofisi ni mambo muhimu ya kumfanya mfanyakazi aridhike na mazingira yake ya kazi”

Mwisho wa kunukuu maneno ya msomi wa enzi hizo ndugu Fredrick Herzeberg, ambaye alikuja kumwagia zege nadharia iliyofanyiwa utafiti mwaka 1927 mpaka 1932 na Profesa Elton Mayo.


Profesa alifanya utafiti wa kuchunguza mazingira ya kazi na tija, pindi alipoona mfumo wa kuwaweka watu wengi wenye historia tofauti katika eneo moja la kazi.

 Alisisitiza kuwa mahusiano mazuri kazini huongeza tija ya kazi, kwani utendaji wa kila siku wa wafanyakazi unategemea sana mahusiano baina yao.

ONYESHA MTAZAMO CHANYA

Kuna kampeni ya usafi Dar es Salaam ina msemo usemao “Usijifanye mstaarabu bali kuwa mstaarabu”. Hata katika mtazamo pia unapaswa usijifanye una mtazamo chanya bali waoneshe wenzako kwa vitendo kuwa wewe una mtazamo chanya.

Mathalani mfanyakazi mwenzako amekumbana na tatizo katika utendaji wake na anaonyesha kuchanganyikiwa ila wewe ukawa mtuliza dhoruba kwa kuwa chanya na tatizo lake na kumpa njia mbadala za kutoka.

Nakwambia ukiwa hivi utakuwa unawavutia wenzako kuja kwako pindi wanapokumbana na changamoto.

 ONYESHA SURA YA FURAHA KILA UTAPOTOA SALAMU

Unawezaje kuingia ofisini macho chini, umeshusha mabega, bila hata ya kutoa salamu na unaenda moja kwa moja kuanza kazi?

Kama hii ndio tabia yako, utaendelea kuwaona wafanyakazi wenzako wakikuchunia au hata kukukwepa kila wakikuona.

Kuwa na tabia ya kutoa salamu kila unapokutana na wafanyakazi wenzako huku ukionyesha uso wa furaha, hii itawapa ishara wenzako kuwa unafuraha kuwa nao eneo moja la kazi.

        JIBU BARUA PEPE NA UJUMBE WA SIMU KWA WAKATI


  Utajisikiaje pale ambapo umemtumia mtu ujumbe uwe wa barua pepe au ujumbe wa kawaida wa simu na anachukua muda mrefu kukujibu au asijibu kabisa?

  Hii itaonyesha una dharau kwa wenzako, na kwamba wao hawana umuhimu kwako. Jenga tabia ya ukarimu wa kujibu ujumbe wa mtu kwa wakati, hii itakufanya uonekane unajali na itawapa urahisi wao kukushirikisha taarifa muhimu kwa wakati.

        KUBALI UTANI ENEO LA KAZI

Simaanishi ukubali kila utani utakaotaniwa hata ule unaovuka mipaka, bali ule utani ambao ni wa kawaida usiovuka mipaka upalilie ili uwafanye wenzako wafurahie uwepo wako kwani dhumuni kubwa la utani ni kufurahi pamoja.

Usishangae mtu huna hata mazoea nae ila akaanza kukutania, hii ina maanisha anataka kupata picha wewe ni mtu wa namna gani. Hasa ukizingatia kuwa ishazoeleka kuwa mtu wa utani ni rahisi kuingilika kwa maongezi na si mtu wa kukasirika hovyo.

       TENGENEZA UAMINIFU

Unapokutana na wengine eneo la kazi hakuna anayejua kuwa wewe ni muaminifu mpaka utakapofanya tendo la uaminifu mbele yao. Hata siku moja mtu asikwambie kuwa yeye si mwizi kama eneo au mazingira anayoishi hakuna cha kuiba. 

Vivyo hivyo huwezi kuwaambia watu wewe ni muaminifu na mkweli kama haujawahi kuonyesha mbele yao tukio la uaminifu na ukweli.

Mathalani endapo umekosea jambo Fulani na ukakubali na kukiri mbele ya wenzako, hii itawajengea picha kuwa wewe ni muaminifu na msema kweli.

        KUWA MTU WA KUTOA MSAADA KWA WENZAKO

Kutoa msaada wa maarifa na utaalamu katika eneo la nje ya muongozo wako wa kazi ni msaada tosha kwa mfanayakazi mwenzako mwenye kuhitaji msaada wako.

Kwa mfano wewe unafahamu kutengeneza kitu Fulani ambacho mfanyakazi mwenzako unamuona kimemuharibikia na anashindwa kukitengeneza, ukijitokeza kumsaidia utakuwa umeimarisha uhusiano wako na yeye na atakuona ni mtu mzuri kuishi nae eneo moja la kazi.

        HESHIMU TOFAUTI ZA UTAMADUNI KATI YAKO NA WENZAKO

Mazingira ya kazi katika zama hizi yameendelea kuwaleta pamoja watu wenye historia tofauti, kuanzia malezi mpaka jamii wanazotokea.

Jinsi wewe unavyokuwa unatumia muda wako na kiwango cha umakini lazima kitatofautiana na wenzako.

Usiwe mtu wa kujilinganisha na kuwaona wenzako ni watu wa ajabu kwakuwa hawapo kama wewe, bali fungua masikio na macho yako kujifunza kitu kutoka kwao ambacho wewe huwezi kukifanya kama wao.

Unapokuwa mtu wa kuheshimu tofauti zako na za wengine, utawafanya na wao watamani kujifunza kitu kutoka kwako, hivyo kuimarisha mahusiano yenu eneo la kazi.

 KUWA NA HESHIMA KWA WOTE

Kama unadhani heshima ni kuamkia wakubwa tu hasa wale unaofanya nao kazi, basi nakuomba utafakari upya. Heshima ni nguzo muhimu sana katika kujenga mahusiano bora eneo la kazi. 

Kumheshimu mwenzako ni pamoja na kujua mipaka ya kauli na maneno ya kuongea mbele yake hata kama umemzidi cheo au umri.

Ukiwa na heshima kwa wengine itakusaidia usiwe miongoni mwa watu wanaopenda kujadili watu wengine kwa mabaya. Ukiwaonyesha heshima watavutika kuja kwako na mahusiano yenu yataimarika.

        SHIRIKIANA NA WENZAKO KATIKA VITU WANAVYOPENDA

Muulize mfanyakazi mwenzako kuhusu vitu anavyopenda kufanya, aina ya muziki anaosikiliza, filamu amazoangalia, na hata vitabu anavyosoma. 

Baada ya kufahamu angalia chochote ambacho mnaendana shirikiana nae, kwa mfano umegundua anapenda sana kuangalia mpira sio mbaya kama ukijiunga nae kama na wewe ni muangaliaji pia.

             SHIRIKI MITOKO NA WENZAKO

Kufahamiana na wafanyakazi wenzako nje ya eneo la kazi ni jambo zuri sana. Ndio maana ofisi nyingi lazima utakuwa kila baada ya muda Fulani wanaandaa tafrija ya kuwakutanisha wafanyakazi katika bonanza ili kujenga mahusiano mazuri baina yao.

Hata kama ofisi haiandai matukio kama hayo ila sio mbaya kama utakuwa unatumia muda wako japo kidogo kutoka na kwenda mahali na wenzako kupata vinywaji au chakula nje ya muda wa kazi ili kuboresha mahusiano mazuri.





Share this post:

Digg it StumbleUpon del.icio.us Google Yahoo! reddit

0 comments:

Post a Comment

 
Copyright 2013-2017 Lisha Ubongo
| Branded by www.pixelbase.co.tz