Ndoa inasemekana ni baraka pale wachumba  wanapokuwa wamependana kwa dhati,
 na kwa hiari yao wanaona ni muda muafaka kuwa kitu kimoja kama mke na mume.
Lakini kwa upande mwingine ndoa inakuwa ni balaa na kupoteza maana pale wachumba wanapoamua kuingia katika ndoa bila sababu za msingi wala vigezo vya maana kati yao.
Yaani kila mmoja anaingia na sababu na mkakati wake tofauti na alionao mwenzake.

Hebu tupeane sababu mbovu kabisa ambazo kama utazitumia kama kigezo cha kufunga ndoa na mtu basi andika umeumia:

1.UMRI WANGU UNAZIDI KUWA MKUBWA:

Hasa wanawake eneo hili ndio linawagusa sana kwani mara nyingi wanajitahidi kukimbizana na muda,
na wanaweka mkakati kabisa kwamba nikifikisha umri fulani lazima niwe ndani ya ndoa.
Ya inawezekana unatumia kigezo cha kuwahi kabla hujapoteza muonekano lakini nakuambia wazi kabisa kama unaingia katika ndoa kwasababu hii, andika maumivu siku zijazo.
Si kwamba usipoolewa basi wewe si mwanamke na kwamba ni mbaya, hapana
ndoa ni taasisi ambayo si kila mtu amepewa uwezo wa kuwa mwanachama kwahiyo ikija nafasi ya wewe kuwa mwanachama ingia bila matatizo lakini si kujidai unakimbizana na muda.


2.MALI AU UTAJIRI WA MWANAUME/MWANAMKE:

Kipindi cha nyuma jamii ilishazoea kwamba mwanamke kuolewa na mtu hata asiyempenda kwa kigezo cha mali za huyo jamaa ni kitu cha kawaida,
lakini bwana siku hizi hadi wanaume nao kigezo hiki wanakitumia ili kutoka kimaisha.
Na ombea huyo unayemdanganya asijue kabla hujafaidika kwani akijua atakuwahi na utakuwa umekosa ulichotaka.
Na wengi wao wanakumbana na mateso makubwa sana wanapoingia katika ndoa na mtu kwasababu ya mali za huyo mwenzake.

3.NILINGANE NA RAFIKI ZANGU:

Sababu hii huwa ni asili kwani mara nyingi binadamu tumekuwa na hulka ya kujilinganisha na wenzetu.
Sasa unapotaka kuingia katika ndoa kwa haraka kwa kuwa tu rafiki yako ameolewa juzi unajitia matatizoni mwenyewe.
Wengi sana wanapata mshawasha pale wanapohudhuria sherehe za harusi za ndugu na marafiki na shamra shamra za ukumbini kwa usiku huo zinawadanganya na kudhani hiyo ndio ndoa na huku kichwani akijenga wazo la yeye pia kutafuta mtu kwa haraka ili afanye kama mwenzake.

4.NJIA YA KUIMARISHA UHUSIANO:

Hapa wengi wanatumia sababu hii kulazimisha ndoa pale wanapoona mahusiano yao katika kipindi hicho sio mazuri sana kwahiyo wanaona njia pekee ni kuingia katika ndoa haraka ili kubadilisha mazingira pengine mambo yatanyooka na kumtuliza mwenzake.
Kama utatumia sababu hii kujifunga kitanzi basi umeingia chaka kwani sio sababu ya msingi kukufanya ulazimishe ndoa.
Kama katika kipindi hiki cha uchumba mnatofautiana si kwamba ndoa ndio itawafanya muwe na mtazamo mmoja kihisia na maamuzi.

5.NATAKA TUWE KARIBU ZAIDI:

Wachumba ambao wanaishi mbali mbali wanadhani kuingia katika ndoa haraka ni njia ya kumaliza umbali baina yao.
Na maamuzi haya mtu anaweza kuyafanya hata kwa kuhama mji na kuhamia alipo mwenzake na kuanza kulazimisha ndoa hata kama mwenzake hajaonyesha utayari.
"Oh! nimechoka kuwasiliana naye kwenye simu kila siku bora nimfuate huko huko aliko na nimlazimishe anioe"
Kweli yawezekana unaumia lakini lazima uzingatie umbali wenu unaletwa na nini,
 na ukishagundua shirikiana na huyo mwenzako namna ya kutatua ndio utajua kama na yeye yuko tayari na huo mpango wako au la
na sio kumvamia alipo na kulazimisha mambo.

6.NIONDOKE KATIKA NYUMBA YA FAMILIA:

Sababu nyingine mbovu ni hii hapa na jua wazi si sababu nzuri kuitumia ili kuingia katika maisha ya ndoa.
Kuwa na subira ni kitu kizuri, 
kama uliweza kulelewa hapo nyumbani kwenu kwa miaka mingi ndoa isiwe kigezo cha kukuondoa.
Kweli kiumri umekua na unatamani uwe kwako ambako utakuwa una maamuzi ya leo unafanya nini au unapika nini.
Na hapa inatokea mara nyingi pale msichana anapotembelea sehemu anayoishi mvulana na kukuta jamaa kiasi fulani kajipanga na anatamani ahamie hapo haraka kwa kumlazimisha ndoa,
 kwani anaona kashapata njia ya mkato. 

7.KISASI KWA ULIYEACHANA NAYE:

Hapa napo wananasa wengi sana, 
yaani utakuta mtu anaachana na mchumba mwezi mmoja nyuma na kwakuwa alimpenda na anataka kumlipizia kisasi basi analazimisha kuingia katika ndoa na mtu mwengine ambaye hajakaa naye hata mwaka kumfahamu.
Hii ni moja ya sababu ya kijinga zaidi kutumia ili kufunga ndoa kwa haraka,
kwani hautakuwa unamkomoa huyo unayetaka umkomoe bali utakuwa unajiingiza katika matatizo wewe mwenyewe.

NDOA NI KITU KIZURI KATIKA MAISHA PALE INAPOKUWA IMEUNGANISHWA NA UPENDO WA DHATI,
UVUMILIVU NA MALENGO SAWA BAINA YA WANANDOA.

JINSIA, HESHIMA AU UTU WAKO HAUTATAMBULISHWA NA NDOA YA KULAZIMISHA ISIYO NA MALENGO SAHIHI.
KUWA MVUMILIVU NA UVUTE SUBIRA,
KAMA UNASTAHILI KUINGIA KATIKA NDOA UTAINGIA TU LAKINI USILAZIMISHE.

Share this post:

Digg it StumbleUpon del.icio.us Google Yahoo! reddit

0 comments:

Post a Comment

 
Copyright 2013-2017 Lisha Ubongo
| Branded by www.pixelbase.co.tz